Sunday, April 16, 2017

UNABII WA UJIRA

“Wakiiacha njia iliyonyoka, wakapotea, wakiifuata njia ya Balaamu, mwana wa Beori, mtu ambaye hakuwa na kipingamizi chochote kwa uovu ilimradi ungelimpatia ujira” (2 Petro 2:15, Fasiri ya Phillips).

Wakati fulani Balaamu alikuwa mtu mwema na pia nabii wa Mungu; lakini sasa alikuwa ameasi, na alikuwa amejiingiza katika tamaa; hata hivyo bado alidai kuwa mtumishi wa Mungu Mkuu. Hakuwa mtu asiyejua utendaji wa Mungu kwa ajili ya Israeli; na wale wajumbe walipomweleza ujumbe waliokuja nao, alifahamu vyema kuwa ulikuwa wajibu wake kukataa zawadi za Balaki na kuwaondosha hao mabalozi. Lakini alithubutu kuchezacheza na majaribu, akawahimiza wajumbe hao wakae pamoja naye usiku huo, huku akitamka kuwa asingeliweza kutoa jibu lolote la hakika hadi atakapokuwa ameomba mashauri ya Bwana. Balaamu alijua kuwa laana yake isingeweza kuwadhuru Israeli. Mungu alikuwa katika upande wao, na kadiri walivyodumu kuwa waaminifu Kwake hakuna uwezo wowote mwovu wa kidunia au jehanamu ambao ungeweza kuwashinda. Lakini kiburi chake kilidanganywa kwa maneno ya wale wajumbe, “Yeye umbarikiye hubarikiwa, na yeye umlaaniye hulaaniwa.” Rushwa ya zawadi za thamani na matarajio ya kutukuzwa viliamsha tamaa yake. Alikubali kwa ulafi hazina zilizoahidiwa kwake, na kisha, wakati akidai kuwa mtii kamili kwa mapenzi ya Mungu, alijaribu kukubaliana na matakwa ya Balaki….
Dhambi ya tamaa ya mali, ambayo Mungu anaitaja kama ibada ya sanamu, ilikuwa imemfanya kuwa mhanga wa mazingira, na kupitia kosa hili moja Shetani alipata nafasi ya kumtawala kabisa. Hili ndilo lililosababishia uangamivu wake. Daima yule mjaribu anaendelea kuwasilisha manufaa na heshima za kiulimwengu ili kuwashawishi watu waache utumishi wa kazi ya Mungu. Anawaambia kwamba uangalifu wao uliopita kiasi ndio unaowazuia wasipate mafanikio. Kwa namna hiyo wengi wanashawishika ili kuthubutu kutoka kwenye njia ya uadilifu kamili. Hatua moja mbaya huifanya nyingine kuwa rahisi zaidi, na huendelea kuwa na ufidhuli zaidi na zaidi. Watafanya na kuthubutu mambo ya kutisha sana mara wanapokuwa wamejiingiza mara moja chini cha utawala wa ulafi na tamaa ya ukuu. Wengi hujidanganya kwamba wanaweza kutoka kwenye uadilifu kamili kwa muda fulani,… na baada ya kufanikisha lengo lao, wanaweza kubadilisha mwenendo wao wakati watakapoona kuwa vyema. Watu wa namna hiyo wanajifunga wenyewe katika mtego wa Shetani, na ni kwa nadra kwamba watajinasua.

No comments: